RAIS SAMIA KUFUNGUA MKUTANO WA KIMATAIFA WA UWEKEZAJI SEKTA YA MADINI - MAGENDELA BLOG

Breaking

Recent-Post

ads header

Thursday, November 14, 2024

RAIS SAMIA KUFUNGUA MKUTANO WA KIMATAIFA WA UWEKEZAJI SEKTA YA MADINI


NA MAGENDELA HAMISI

 

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan, anatarajia kufungua Mkutano wa Sita wa Kimataifa wa Uwekezaji katika Sekta ya Madini utakaoanza Novemba 19 mwaka huu jijini Dar es Salaam na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt Hussein Alli Mwinyi ataufunga Novemba 21, 2024.

 

Aidha Mkutano huo mkubwa wa Madini unatarajiwa kuudhuriwa na washiriki zaidi ya 1,500 kutoka mataifa mbalimbali Duniani ambapo wataalamu, Mawaziri, mabalozi watafiti watashiriki mkutano huo na watajadili mada nane kutoka watoa mada 20 wa kimataifa na 35 wa hapa nchini ambao wamebobea kwenye sekta ya madini.

 

 

Waziri wa Madini Antony Mavunde, amebainisha hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari na kufafanua kuwa kwa mdau anayetaka kushiri anaweza kujisajili kupitia tovuti ya mkutano ambayo ni conference.madini.go.tz.

 

 

“Tunamshukuru Rais Dk. Samia kupitia mikakati yake amefanikisha sekta ya madini kupiga hatua kibwa kimafanikio na sasa inachangia katika pato la taifa asilimi tisa na mkakati ambao upo kwa sasa ifikie asilimia 10 na Novemba 19 atafungua mkutano huo na utafungwa na Rais wa Zanzibar Dkt Mwinyi,” amesema.

 

Ameongeza kuwa wadau mbalimbali wataudhuria mkutano huo wakiwemo, Watendaji Wakuu wa kampuni kubwa za madini duniani ambazo zinatarajia kuwekeza nchini, ikiwemo Kampuni ya Barrick Gold, AngloGold Ashanti, Life Zone Metals, ShantaGold, Eco Graph, Faru Graphite, HeliumOne, Lindi Jumbo, Sotta Mining.

 

Pia amesema wengine watakaokuwemo ni watafiti, mabalozi 31 wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini na wanaoiwakilisha nchi yetu nje ya nchi akiwemo Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Umoja wa Mataifa, Balozi Hussein Kattanga, Mashirika ya Kimataifa, waongezaji thamani madini, wafanyabiashara, taasisi za fedha, Vyuo Vikuu na Vya kati, Taasisi za umma na binafsi zinazojihusisha na shughuli za madini, viongozi mbalimbali wa kitaifa kutoka wizara, Taasisi, Mikoa, Halmashauri na Idara za Serikali.


Waziri Mavunde amesema mkutano huo amewahamasisha wadau na watanzania kutumia fursa ya uwepo wa mkutano huo kujifunza, kufuatilia na kushiriki ili kuijenga uchumi wa nchi kupitia shughuli mbalimbali katika mnyororo wa thamani kwenye sekta ya madini.



Ameweka wazi kwamba mkutano huo unalenga si tu kuvutia uwekezaji, bali pia kuweka msingi thabiti wa ushirikiano baina ya wadau, kuimarisha uzalishaji wa madini, na kuhakikisha kuwa rasilimali hizi zinawanufaisha watanzania kiuchumi na kijamii.



Mada zitakazojadiliwa zitagusia maeneo mengi ikiwemo changamoto zinazokabili masuala ya uongezaji thamani madini, fursa za uwekezaji na mitaji kwenye sekta ya madini; mikakati ya uendelezaji madini mkakati kwa ajili ya kuongeza manufaa ya mnyororo wa thamani, matumizi ya teknolojia katika uchimbaji mdogo wa madini; ushiriki wa wanawake na vijana katika Sekta ya madini, kuendelea kutangaza madini adimu ya Tanzanite, na masuala mengine yakiwemo uchimbaji bora na uhifadhi wa mazingira.




Mkutano huo utaongozwa na kaulimbiu isemayo “Uongezaji thamani Madini kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii”, ambayo inalenga kuhimiza umuhimu wa uongezaji thamani wa madini kama njia ya kuleta faida zaidi za kiuchumi na kijamii kwa maendeleo endelevu ya taifa letu na dunia.

 

Pia utakuwana mkakati wa kupandisha thamani ya madini yanayozalishwa nchini kabla ya kusafirishwa nje kwa lengo la kuchochea uanzishwaji viwanda vitakavyokuwa na manufaa nchini, kwa majirani wanaotuzunguka na duniani.


Ameongeza kuwa Novemba 20, 2024 kutakuwa na hafla ya usiku wa madini itakayofanyikakuanzia Saa 12.30 Jioni na mgeni rasmi  atakuwa ni  Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati wa Tanzania, Dkt. Doto Biteko.


Wazizri Mavunde ametanabaisha kuwa katika hafla hiyo kutakuwa na tukio maalum la kutambua mchango wa wadau waliofanya vizuri katika sekta ya madini kupitia makundi mbalimbali.

 

Pia hafla hiyo inalenga kutambua mchango wa wadau hawa katika maendeleo na ukuaji wa sekta, huku ikihamasisha wadau wengine kuongeza juhudi, kuziona fursa zilizopo na kuchangia katika mafanikio ya sekta ya madini nchini. Pia, usiku wa madini huambatana na onesho la bidhaa za madini ya vito.

 

Amesema mkutano huo ni mwendelezo wa mikutano mingine iliyotangulia tangu kuanza kwake mwaka 2019 ambapo Serikali ilitenga zaidi ya saa sita kusikiliza kero, changamoto na maoni kutoka kwa wadau wa madini. 



"Kutokana na matokeo ya mkutano ule wa Mwaka 2019, Serikali iliona umuhimu wa kuwa na mikutano huu yenye sura ya Kimataifa na hivi sasa, imevuka mipaka ya nchi yetu ikihusisha wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania wanaohusika katika mnyororo mzima wa shughuli za madini.



"Kama mnavyofahamu kwamba, nchi yetu ya Tanzania imejaliwa utajiri wa aina mbalimbali za madini kutoka makundi karibu yote ya madini yakihusisha madini ya metali, madini mkakati, madini ya viwandani, vito vya thamani kubwa, madini yanayopatikana chini ya sakafu ya bahari kuu, ambayo yote yanaifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi wazalishaji wakubwa wa madini yanayohitajika duniani kote.



Kwa muktadha huo, Serikali kupitia Wizara ya Madini iliona upo umuhimu wa kuwa na jukwaa moja  linalowaleta pamoja wadau kutoka pande mbalimbali za nchi  kusikia kutoka kwetu moja kwa moja kuhusu uwepo wa rasilimali hizi  ambapo ikiwa zitatumika vizuri zinaweza kuibadili kiuchumi na kijamii Nchi yetu ya Tanzania na kuifanya moja ya Nchi zinazozalisha kwa wingi madini  duniani." Ameeeleza

 

Amesema mkutano huo unafanyika kila mwaka ili kuimarisha mazingira ya uwekezaji na kuendelea kuvutia wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.



Pia ni jukwaa la kujadili kwa pamoja mustakabali wa sekta ya madini, kushirikishana maarifa, ujuzi na kuangazia fursa mpya zinazojitokeza katika sekta hii inayokua kwa kasi. 



Aidha mkutanmo huo unatoa nafasi kwa washiriki kujifunza kuhusu Sera na mikakati mipya ya serikali, kujadili masuala ya kisheria na kiuchumi yanayohusiana na madini, na kushuhudia teknolojia mpya na ubunifu unaoweza kuleta thamani zaidi katika utafiti, uchimbaji  na uongezaji thamani wa madini kupitia mawasilisho na maonesho kwenye mabanda yanayoenda sambamba na mkutano.








 

 


No comments:

Post a Comment