THAMANI YA MIRADI YA RAIS SAMIA KWENYE SEKTA YA MISITU NA NYUKI KWA JAMII IMEONEKANA - BUNGE - MAGENDELA BLOG

Breaking

Recent-Post

ads header

Wednesday, November 13, 2024

THAMANI YA MIRADI YA RAIS SAMIA KWENYE SEKTA YA MISITU NA NYUKI KWA JAMII IMEONEKANA - BUNGE


NA JOHN MAPEPELE

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili  na Utalii imesema imeona thamani ya fedha  ambayo Serikali  kupitia   Wizara ya Maliasili na Utalii  imewekeza kwenye sekta ya misitu na nyuki.



Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mheshimiwa Timotheo Mnzava (Mb) amesema haya   leo Novemba 13, 2024 wakati anahitimisha  ziara ya kikazi  mkoani Tabora kwenye  kiwanda cha kuchakata mazao ya nyuki cha Nkiniziwa wilayani Nzega baada ya  kukagua miradi mbalimbali ya sekta ya misitu na nyuki huku akitaka juhudi zaidi  za kutangaza ziongezwe.


 Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania Prof Dosantos Silayo amesema mradi wa kiwanda hicho umefadhiliwa na  Mfuko wa Misitu Tanzania na  Wakala  wa Huduma  za Misitu Tanzania ambapo hadi kukamilika umegharimu  takribani shilingi milioni 295


Kamati imeielekeza  Wizara kwa kushirikiana na wadau  kuendelea  kuanzisha vikundi vya wajasiliamali  na viwanda vya mazao ya misitu na nyuki ili uzalishaji uongezeke na kupanua ajira kwa wananchi.


Katika ziara hiyo  Kamati iliambatana na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii,  Dunstan Kitandula (Mb), Katibu Mkuu, Dkt. Hassan Abbasi na baadhi ya Watendaji wa Wizara na taasisi  zilizo chini ya Wizara.


Aidha, Mhe. Mnzava  amesema  sekta za misitu na nyuki zina mchango mkubwa kwa jamii hivyo ni muhimu kusimamia kikamilifu utekelezaji wa miradi hiyo.


Amefafanua kuwa endapo sekta ya misitu na nyuki itasimamiwa kikamilifu  ina mchango kwenye uhifadhi wa Maliasili kwa kuwa watu wataacha tabia za kuharibu misitu na mazingira kwa ujumla.


Ameitaka Wizara kuendelea kuwekeza kwenye elimu ya namna bora  ya kufuga nyuki na kuvuna asali kwa njia bora ili kupata bidhaa zenye ubora zitakazopenya kwenye masoko ya kimataifa.


Miradi hiyo inatekelezwa katika Wilaya zote 7 za Mkoa wa Tabora ambazo ni Tabora, Uyui, Nzega, Igunga, Sikonge, Urambo na Kaliua. 


Naye Mhe. Kitandula kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi. Dkt. Pindi Chana ameishukuru kamati kwa ushauri na maelekezo iliyoyatoa  na kuahidi kuyatekeleza kikamilifu.


Mara baada ya kuhitimisha ziara hiyo, Mhe. Mnzava amepanda mti katika eneo la kiwanda ikiwa ni ishara ya kuendeleza uhifadhi.







No comments:

Post a Comment