KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Agosti 14, 2026 imepitia na kuujadili mkakati wa kuimarisha huduma za Maji, lishe, upandaji wa miti na utunzaji wa mazingira kwenye shule za msingi na Sekondari nchini, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea Mkutano wa Nne wa Bunge unaotarajiwa kuanza Agosti 25, 2026.
Katika kikao hicho, Kamati imejadili kwa kina namna bora ya uimarishaji wa huduma za maji , upandaji wa miti na utunzaji wa mazingira kwenye Shule za msingi na sekondari nchini, pamoja na uimarishaji wa lishe katika shule za msingi nchini.
Mara baada ya kuupitia mkakati huo, Kamati kupitia Mwenyekiti wake Florent Kyombo, katika eneo la lishe imeitaka OWM - TAMISEMI kufanya utafiti wa kina ili kuwa na takwimu halisi za lishe mashuleni, kuimarisha somo la kilimo mashuleni ili kuwapatia ujuzi wa kilimo wanafunzi, ikiwa ni pamoja na kupata chakula cha kutosha mashuleni.
Kwa upande wa upandaji miti na utunzaji wa mazingira, Kyombo ameitaka OWM - TAMISEMI kuhakikisha shule zinakuwa na vilabu mahususi za upandaji miti, kuwa na mkakati wa kupanda miti mashuleni na kila shule kupata mgawo wa miche na kuongeza kuwa, shule ziwekewe ukomo wa idadi ya miti inayotakiwa kupandwa kila mwaka.
Ili kuimarisha huduma za maji mashuleni, Mhe. Kyombo ameitaka OWM - TAMISEMI kuhakikisha miundombinu ya maji iliyopo mashuleni inatunzwa, kusimamia utaratibu wa ulipaji wa bili za maji mashuleni kwa wakati na kuongeza kuwa kila shule kuwe na sharti au utaratibu wa kuchimba kisima au kuweka tanki la maji ili wanafunzi wawe na uhakika wa huduma ya maji.










No comments:
Post a Comment