Na James K. Mwanamyoto, Dar es Salaam
Tarehe 18 Februari, 2023
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na
Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amemtembelea Mama Salma Omar,
mjane wa Hayati Dkt. Omar Ali Juma, aliyekuwa Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa
majukumu yake ya kuwahudumia viongozi wastaafu wa kitaifa na wajane
wa viongozi hao.
Mhe. Jenista amesema, amefika nyumbani kwa Mama Salma jijini Dar es
Salaam kwa lengo la kumjulia hali na kutambua mchango wa Hayati Dkt.
Omar Ali Juma aliuotoa katika kulijenga taifa wakati wa uhai wake.
“Nimekuja kukutembelea kwa lengo la kukujulia hali, tuzungumze, nipate
busara zako na kujua changamoto unazokabiliana nazo ili tuzitafutie
ufumbuzi kwani mzee pamoja na wewe mmetoa mchango mkubwa katika
maendeleo ya taifa hili.” Mhe. Jenista amefafanua.
Aidha, Mhe. Jenista amewasilisha salamu za heri kwa mama Salma Omar
kutoka kwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia
Suluhu Hassan, Makamu wa Rais, Mhe. Dkt. Phillip Isdor Mpango na
Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa.
Sanjali na hilo, Mhe. Jenista amemtakia heri ya siku ya kuzaliwa Mama
Salma Omar kwa kumpatia zawadi ya ua ikiwa ni ishara ya upendo na
kumtakiwa maisha marefu.
Kwa upande wake, Mama Salma Omar, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kitendo cha
Serikali yake kuendelea kuwahudumia wajane wa viongozi wastaafu wa
kitaifa.
Mhe. Jenista Mhagama anaendelea na utaratibu wake wa kuwatembelea
viongozi wastaafu wa kitaifa na wajane wa viongozi hao ambao wameacha
alama kubwa katika taifa kwa mchango walioutoa wakiwa madarakani.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akimpa zawadi ya ua mama Salma Omar mjane wa hayati Dkt. Omar Ali Juma aliyekuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwa ni ishara ya kumtakia heri ya siku ya kuzaliwa alipomtembelea nyumbani kwake jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na mama Salma Omar mjane wa hayati Dkt. Omar Ali Juma aliyekuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipomtembelea nyumbani kwake jijini Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiagana na mama Salma Omar mjane wa hayati Dkt. Omar Ali Juma aliyekuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipomtembelea nyumbani kwake jijini Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake.




No comments:
Post a Comment