WAZALISHAJI MALI JESHI LA MAGEREZA WATAKIWA KUONGEZA JITIHADA - MAGENDELA BLOG

Breaking

Recent-Post

ads header

Wednesday, March 15, 2017

WAZALISHAJI MALI JESHI LA MAGEREZA WATAKIWA KUONGEZA JITIHADA

Suleiman Msuya

WAKUU wa Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Magereza Tanzania wametakiwa kuongeza jitihada za uzalishaji na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji kila miezi mitatu kwa katibu mkuu wa wizara ya mambo ya ndani ya nchi.


Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Manunuzi wa Wizara ya Mambo ya Ndani nchini, David Mwangosi wakati akizungumza na makamanda wa shirika hilo jana katika Ukumbi wa Bwalo Kuu la Maofisa Ukonga jijini Dar es Salaam.

Mwangosi alisema shirika hilo linapaswa kuwa chachu ya uzalishaji wa mazao ili yaweze kutosheleza wafungwa na jamii nyingine.

Alisema iwapo kila kiongozi atasimamia majukumu yake na kuongeza uwajibikaji ni wazi kuwa uzalishaji utaongezeka hivyo kutimiza matarajio ya Serikali ya kuifikisha Tanzania ya viwanda na uchumi wa kati.

Mkurugenzi huyo alisema kila viongozi ambao wanasimamia shirika hilo wanapaswa kuwa wabunifu kwa kushawishi wadau mbalimbali ili kuweza kushirikiana katika miradi mbalimbali.

“Nimekuja hapa kumuwakilisha Katibu Mkuu, Meje Jenerali mstaafu Projestus Rwegasira na amesema hataki mzaha katika kazi anataka kila baada ya miezi mitatu muwe mnamletea taarifa ya shirika katika kuzalisha,” alisema.

Aidha, mkurugenzi huyo amewataka makamanda wote ambao wanasimamia shirika na miradi kuhakikisha kuwa wanaanzisha viwanda vidogo vidogo kwani ni chachu ya maendeleo.

Mwangosi alisema wizara ipo tayari kuunganisha Jeshi la Magereza Tanzania na nchi mbalimbali ambazo zinaweza kusaidia uanzishaji wa viwanda vidogo.
Alisema wizara ipo tayari kutoa mafunzo iwapo itahitajika hasa kwa wafungwa ambao watakuwa wanatumiwa katika viwanda husika.

Kwa upande mwingine mkurugenzi huyo wa manunuzi alisema wapo katika harakati za kulipa madeni yote ambayo yamewasilishwa kwao ili kuondoa migogoro na wadai.
Alisema pamoja na kuahidi kulipa madeni hayo pia aliwataka waandaaji wa taarifa kuzingatia usahihi ili kuepuka kusumbuliwa mara kwa mara kutokana na kutoeleweka.

Kwa upande wake Kamishna Jenerali wa Magereza (CGP), Dk. Juma Malewa alisema jeshi hilo lina miradi takribani 23 ya uzalishaji hivyo wanajipanga ili miradi hiyo iwe na tija.
Alisema shirika hilo linajihusisha na uzalishaji wa mahindi, maharage, mpunga, alizeti, maziwa na nyama ambapo kutokana na changamoto mbalimbali yapo maeneo ambayo hajafanya vizuri.

Dk. Malewa alisema kutokana na uhaba wa fedha na kuchelewa kwa ruzuku uzalishaji wa mbegu bora za kilimo umekuwa ukishuka  mwaka hadi mwaka

“Mhemiwa mgeni rasmi shughuli za uzalishaji katika miradi ya viwanda vidogo vidogo zimeendelea kufanya vizuri pamoja na changamoto za uchakavu wa mashine na mitambo,” alisema.

Alisema kutokana na maendeleo ya teknolojia viwanda vilivyopo vinahitaji mashine na mitambo ya kisasa ili kukidhi uzalishaji wa bidhaa na ushindani katika soko.

Kamishna Malewa alisema shirika linaendelea kutoa chakula kwa wafungwa ambapo hadi kufikia Januari lilikuwa limefika zaidi y ash. bilioni 3.6 na deni kwa taasisi za Serikali likifikia  zaidi ya sh. bilioni 3.

Dk. Malewa alisema kwa sasa wanashirikiana na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa (NSSF) na (PPF) kuendeleza shamba la miwa na Kiwanda cha Sukari Gereza la Mbigiri na pia wanarajia kuendeleza s Shamba la Mbegu Bagamoyo lenye ekari 200.


No comments:

Post a Comment