NA MWANDISHI WETU, SAME
MKUU wa Wilaya ya Same Kasilda Mgeni, ametoa mwezi
mmoja kwa uongozi wa halmashauri hiyo kuhamisha gulio linalofanyika Jumatano
hadi Jumapili eneo lililotengwa kwa ajili ya Viwanja vya Michezo Maarufu
Kwasa-Kwasa.
Ametoa maagizo hayo wakati akizungumza na
wafanyabiashara wa Soko hilo ikiwa ni mwendelezo wa ziara zake kusikiliza
na kutatua kero mbalimbali za wananchi wa Wilaya ya Same ambapo amesisitiza
uboreshwaji wa miundombinu kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara.
Alisema kitendo cha halmashauri kuruhusu eneo la
michezo kutumika kama gulio hakikubaliki kwani kinarudisha nyuma jitihada za
serikali kukuza michezo.
Mkuu huyo wa wilaya alisema wanamichezo wamekuwa
wakilalamika ila hawasikilizwi hivyo anatoa mwezi mmoja kwa halmashauri kupata
ufumbuzi wa kero hiyo.
Kwa upande mwingine DC Kasilda ameeleza
kutoridhishwa na hali ya Soko Kuu la Mji wa Same kutokana na uchafu
uliokithiri, vyoo vinavyotumika kukosa ubora unaohitajika hivyo kuhatarisha
usalama wa afya za wafanyabiashara na wanunuzi wanaotumia soko hilo na kuagiza
halmashauri kukarabati haraka iwezekanavyo.
Awali wafanyabiashara wa soko hilo wakitoa
malalamiko yao wamemweleza mkuu huyo wa wilaya kuwa soko hilo linakabiliwa na
ubovu wa miundombinu, kama mashimo makubwa yaliyo ndani ya soko, kukosekana
umeme hali inayosababisha kuendesha biashara kwa shida wakitaharisha pia
usalama wao.
No comments:
Post a Comment