CHALAMILA APANGA MKAKATI WA UJENZI WA RELI ZA NDANI KUONDOA SHIDA YA USAFIRI DAR - MAGENDELA BLOG

Breaking

Recent-Post

ads header

Thursday, January 30, 2025

CHALAMILA APANGA MKAKATI WA UJENZI WA RELI ZA NDANI KUONDOA SHIDA YA USAFIRI DAR


NA MWANDISHI WETU

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amesema anatarajia kufanya mazungumzo na Halmashauri ya Jiji na Shirika la Reli (TRC) kujadili uwezekano wa kujenga reli za ndani mkoani humo. 

Amesema lengo la majadiliano hayo ni kuhakikisha reli inajengwa kupitia makusanyo ya kodi ya mkoa huo na ikiwa mchakato huo utakamilika itafanikisha kupunguza adha ya usafiri mkoani humo.

"Naamini tukikaa na Wadau mbalimbali wakiwemo TRC na Halmashauri ya Jiji kujadili suala hili tunaweza kupata majibu sahihi ya gharama ya ujenzi huo wa reli na tutatumia makusanyo ya kodi kufanikisha ujenzi huo," amesema.

Amebainisha hayo Januari 30, mwaka huu jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na Waandishi wa habari ambapo pia alimshukuru Rais Samia kwa kufanikisha Mkutano wa Nishati kwa nchi za Afrika na Marais zaidi ya 20 waliudhuria.

"Namshukuru Rais Samia kwa kufanikisha mkuu huo mkubwa ambao kwa kiasi kikubwa umeitangaza nchi na Mkoa wa Dar es Salaam kwa ujumla," amesema

Pia amewashukuru na kuwapongeza wananchi wa Mkoa huo kwa ushirikiano mkubwa walioutoa ikiwemo kuimarisha amani, utulivu na usafi wakati wote WA Mkutano huo.

Vilevile akizungumzia suala la ujenzi wa soko la Kariakoo Chalamila amesema zaidi ya bilioni 28 zimetolewa na Rais Dokta Samia Suluhu kwa ajili ya ujenzi wa soko  hilo na kwamba ujenzi wake umefikia asilimia 97 pia amesema kwa sasa bodaboda na bajaji hazijazuiliwa kuingia katikati ya jiji kwani walizuiwa kwa siku chache    kutokana na ugeni wa marais wa Afrika.


Wakati huo huo, Chalamila ametangaza rasmi kuanza kwa shughuli za biashara kwenye jiji hilo saa 24 ambapo uzinduzi rasmi utafanyika Februari 22 mwaka huu kwani jiji hilo ni muhimu kwenye ukuaji wa uchumi.



Sanjari na hilo kwa upande wa Mwenyekiti wa bodi ya soko la kariakoo Hawa Ghasia amesema kuanzia januari 31 wanaanza kuweka majina ya wafanyabiaahara ambao walikuwepo kwenye soko la kariakoo kabla halijaungua ili wasajiliwe na kwamba baada ya hapo watasajili wafanyabiashara wapya na waliokuwa wanadaiwa wanapaswa kulipa madeni yao.

No comments:

Post a Comment