NA MWANDISHI WETU
BARAZA la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO) limetangaza kufanyika kwa Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali 2026, litakalowakutanisha zaidi ya washiriki 3,000 kutoka ndani na nje ya Tanzania kujadili mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya taifa.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Jukwaa hilo, Jasper Makala, amesema mkutano huo utafanyika kuanzia Oktoba 20 hadi 22, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma.
Amesema jukwaa hilo linaandaliwa kwa ushirikiano kati ya NaCoNGO na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, likiwa na lengo la kuimarisha ushiriki wa mashirika yasiyo ya kiserikali katika kuleta maendeleo endelevu kwa jamii na taifa kwa ujumla.
Amesema jukwaa hilo litawakutanisha wanachama wa mashirika yasiyo ya kiserikali, viongozi wa serikali, sekta binafsi, washirika wa maendeleo, vyombo vya habari na wadau wengine muhimu kwa lengo la kujadili mustakabali wa sekta hiyo na mchango wake katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Pia jukwaa hilo litakuwa na mijadala mbalimbali itakayojikita katika namna mashirika yasiyo ya kiserikali yanavyoweza kuongeza ufanisi wa utendaji wake na kuimarisha mchango wake katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.





No comments:
Post a Comment