WADAU KILIMO WAJADILI CHANGAMOTO - MAGENDELA BLOG

Breaking

Recent-Post

ads header

Thursday, September 25, 2025

WADAU KILIMO WAJADILI CHANGAMOTO


NA MWANDISHI WETU

WADAU wa kilimo duniani wametumia mkutano wa kimataifa wa haki za

wakulima kujadili namna kifungu cha tisa cha Mkataba wa Kimataifa wa

Rasilimali za Vyakula na Kilimo (ITPGRFA), unavyoweza kushughulikia

changamoto wakati wa dharura, ikiwamo misukosuko ya kisiasa na

majanga ya asili.

Katika mkutano huo wa pili uliofanyika hivi karibuni jijini Manila,

Ufilipino, taasisi zisizo za Serikali nchini, ziliwakilishwa na mtaalamu wa

sera na utafiti kutoka Mtandao wa Baionuai (TABIO), Daud Manongi.

Manongi alisema mkutano huo pamoja na mambo mengine, hoja ya

dharura kuhusu mustakabali wa wakulima ilitawala mijadala.

Alisema katika mjadala huo, mataifa yaliyotajwa kuathiriwa na

misukosuko ya kisiasa ni pamoja na Sudan, Sudan Kusini, Jamhuri ya

Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Myanmar na Haiti.

Mtaalamu huyo alisema athari za majanga ni vimbunga, ukame na

milipuko ya visumbufu vikijadiliwa kama changamoto kubwa

zinazohatarisha ustawi wa wakulima.

“Kwa mujibu wa hoja hiyo, dharura hizi zimekuwa zikisababisha,

uharibifu wa mifumo ya mbegu na mazao, kupotea kwa maarifa ya jadi

ya kilimo, wakulima kushindwa kuhifadhi, kutumia, kubadilishana na hata

kuuza mbegu kipindi ambacho wanazihitaji zaidi,” alisema.


Alisema bila mikakati mahsusi, urejeshaji wa mifumo hii huchukua muda

mrefu na mara nyingi hukosa usawa, jambo linalosababisha ukosefu wa

haki kwa wakulima wadogo.

“Katika majadiliano hayo, ilisisitizwa kuwa ni lazima kuwe na malengo ya

moja kwa moja, yanayolenga kuwezesha urejeshaji haraka wa uzalishaji,

kuimarisha benki za mbegu za kijamii, kulinda na kudumisha maarifa ya

jadi ya wakulima,” alisema.

Alisema Sekretarieti ya Mkataba wa ITPGRFA ilikubali kuwa mfuko wa

dharura upo, lakini ikabainisha kwamba bado kuna haja ya kuanzisha

malengo yanayoakisi mazingira halisi ya dharura, na kushirikisha jamii

kikamilifu, ili wajisikie kuwa sehemu ya utekelezaji wa haki zao.

Manongi alisema mjadala huo umeonesha dhahiri, kuwa mustakabali wa

haki za wakulima nyakati za dharura, unategemea uwepo wa mikakati

thabiti na jumuishi, itakayowezesha wakulima kuendelea kuwa walinzi wa

urithi wa mbegu na maarifa ya kilimo duniani.




No comments:

Post a Comment